MSHAMBULIAJI wa Simba SC, Kibu Denis, ameaga rasmi klabu hiyo baada ya kuitumikia kwa miaka minne na nusu, akieleza kuwa amepata changamoto mpya ya kwenda “kutengeneza familia” katika klabu ya Al Nasr ya Libya.
Kibu amejiunga na Al Nasr kwa ada ya uhamisho ya dola za Marekani 300,000 (takribani Sh milioni 776) na kusaini mkataba wa mwaka mmoja na nusu.
Akizungumza kwa hisia baada ya kukamilisha uhamisho huo, Kibu aliwashukuru wachezaji wenzake, benchi la ufundi na uongozi wa Simba kwa sapoti waliyompa katika kipindi chote alichokuwa klabuni hapo.
“Nimefanya kazi Simba kwa miaka minne na nusu, nimepata sehemu nyingine ya kwenda kutengeneza familia. Nawashukuru wachezaji wenzangu kwa sapoti waliyonipa kama rafiki, familia na ndugu. Pia, benchi la ufundi. Nawatakia kila la heri msimu huu,” alisema Kibu.
Katika mkataba wake mpya, Kibu anatarajiwa kulipwa jumla ya dola 700,000 (sawa na takribani Sh bilioni 1.8) kwa kipindi chote cha mwaka mmoja na nusu. Kati ya fedha hizo, dola 900,000 ni mshahara na atakuwa akipokea bonasi ya dola 50,000 kwa mwezi kulingana na makubaliano ya kimkataba.
Uhamisho wa Kibu unaongeza idadi ya wachezaji wa Tanzania wanaokwenda kucheza soka la kulipwa Afrika Kaskazini, hatua inayotajwa kuwa ni fursa ya kukuza kipaji chake na kuongeza thamani katika soka la kimataifa.
Kibu ameondoka Simba akiwa ni miongoni mwa wachezaji waliotoa mchango mkubwa ndani ya kikosi hicho katika mashindano ya ndani na kimataifa, akijijengea jina kwa uwezo wake wa kucheza nafasi zaidi ya moja katika safu ya ushambuliaji.
Klabu ya Simba imemtakia kila la heri mchezaji huyo katika safari mpya ya soka nje ya Tanzania.