Al Nasr imefikia makubaliano rasmi na Simba ya kumnunua mshambuliaji Kibu Denis baada ya klabu hiyo ya Libya jana kukubaliana maslahi binafsi na nyota huyo wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’.
Baada ya awali Simba kuonyesha utayari wa kumuuza Kibu Denis, kilichobakia kilikuwa ni makubaliano binafsi baina ya Al Nasr na Kibu Denis ambayo yalichelewa kufanyika kwa vile mchezaji huyo alikuwa Angola akiitumikia Simba katika mchezo wa raundi ya tano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu.
Lakini baada ya nyota huyo kurejea, jana, Jumatatu, Februari 9, 2026, miamba hiyo ya Libya ilikutana na upande wa mchezaji huyo na wakakubaliana rasmi na hivyo mchezaji huyo ataungana na Al Nasr.
Uhamisho huo utaifanya Simba ivune kiasi cha Dola 300,000 (Sh776 milioni) kwa kukubali kumuachia Kibu ambaye mkataba wake ulibakia miezi mitano ufikie tamati.
Msimamizi wa Kibu Denis, Carlos Sylivester amesema kuwa taarifa zozote kuhusu mshambuliaji huyo zitatolewa na Simba.
Ndani ya Al Nasr, Kibu atakutana na nyota wawili aliocheza nao Simba hivi karibuni ambao ni kiungo Fabrice Ngoma na mshambuliaji Steven Mukwala pamoja na Aziz Ki anayecheza Al Ittihad.