HomeKITAIFAMANGUNGU: MABADILIKO YA BENCHI LA UFUNDI NDIO YALIIVURUGA SIMBA

MANGUNGU: MABADILIKO YA BENCHI LA UFUNDI NDIO YALIIVURUGA SIMBA

MWENYEKITI wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu, amesema mabadiliko ya ghafla katika benchi la ufundi yamechangia kwa kiasi kikubwa kutokuwa na mwanzo mzuri wa msimu huu kwa timu hiyo.

Mangungu amesema msimu uliopita Simba ilikuwa chini ya kocha mpya, Fadlu Davids, ambaye alihitaji aina maalumu ya wachezaji watakaokwenda sambamba na falsafa yake ya soka, jambo lililowasaidia kumaliza msimu katika nafasi ya pili na kufika fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Ameeleza kuwa walipoanza msimu huu, uongozi uliingia sokoni kusajili wachezaji kulingana na mapendekezo ya kocha huyo, lakini ujio wa ofa kubwa kwa Davids uliwalazimu kumuacha aondoke, hali iliyovuruga mipango yao mapema.

“Wakati tunaanza msimu na kusajili wachezaji aliowapendekeza, ikaja ofa kubwa kwake na hatukuwa na budi kumzuia. Hilo lilituvuruga sana kwa sababu tulilazimika kuingia sokoni tena kutafuta kocha mwingine,” amesema Mangungu.

Ameongeza kuwa Simba ilifanikiwa kumpata Steve Barker, ambaye naye amekuja na falsafa yake ya uchezaji, hivyo kulikuwa na ulazima wa kufanya usajili mwingine wa wachezaji watakaosaidia timu kufikia malengo yake.

Mangungu amesema ujio wa kocha mpya katikati ya mashindano, pamoja na usajili wa wachezaji wapya, bado ni changamoto kwa timu kutokana na kukosekana kwa muunganiko wa pamoja.

Amefafanua kuwa mafanikio ya timu si juhudi zake peke yake bali ni matokeo ya ushirikiano wa viongozi wengine, hata hivyo lawama nyingi hutupwa kwake pale timu inapofanya vibaya.

“Jambo ninalokubaliana nalo ni waache wapewe sifa wanaowapenda, lakini lawama zije kwangu. Mimi siwezi kufanya timu ifanye vibaya kwa makusudi, kwa sababu tumeunda bodi na menejimenti yenye uwezo wa kufanya kazi na benchi la ufundi au wachezaji,” amesema.

Ameongeza kuwa kulingana na mgawanyo wa majukumu, yeye binafsi hana nafasi ya kukutana moja kwa moja na wachezaji, bali bodi hukaa na kuwasilisha maelekezo kwa menejimenti ili yawafikie wachezaji.

Mangungu amesema kelele na vurugu zinazoshuhudiwa hazichochewi na mashabiki au wanachama wa kweli wa Simba, bali ni watu wachache walioundwa kwa ajili ya propaganda na kuiondoa klabu hiyo kwenye mstari wake.

RELATED ARTICLES

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Most Popular

Recent Comments

Web Development Company in Kochi,Kerala on NEYMAR AMWAGA MACHOZI AKIKUTANA NA KIPIGO KIKUBWA ZAIDI KWAKE