KUNA mchezo mmoja wenye hadhi ya fainali utakaopigwa leo Uwanja wa Amaan kuanzia saa 2:15 usiku na Azam FC itakutana na bingwa mtetezi wa Kombe la Muungano, Yanga, katika nusu fainali ya kwanza ya michuano hiyo.
Yanga ndiyo ilikuwa ya kwanza kufuzu hatua hii baada ya kuifunga Muembe Makumbi City mabao 4-0 katika robo fainali, huku Azam ikifuata siku moja baadaye kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya KVZ.
Yanga inalenga kutetea taji hilo ililochukua msimu uliopita ilipoifunga JKU bao 1-0, wakati Azam ikisaka kuandika historia kwa kushinda ubingwa wake wa kwanza wa Kombe la Muungano.
Msimu huu, timu hizi zimekutana mara mbili. Mara ya kwanza ilikuwa kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi na Yanga ilishinda kwa penalti 5-4 baada ya sare ya dakika 120, na mara ya pili walikutana kwenye ligi na mchezo ulimalizika kwa sare tasa.
Katika ligi kuu, zote bado hazijapoteza mchezo wowote hadi sasa, jambo linaloonyesha uimara wao. Matokeo yao mabaya yamekuwa ni sare pekee, hali inayoongeza ushindani kuelekea pambano hili.
Rekodi zinaonyesha nje ya ligi wamekutana mara 17 katika mashindano mbalimbali; Yanga ikishinda mechi 10, Azam ikishinda tano huku sare zikiwa mbili.
Yanga inatambua kwamba itakuwa na mchezo mgumu dhidi ya Simba, Mei 3 mwaka huu, lakini bado imekuwa haitaki utani ikiwatumia mastaa wake muhimu kama ambavyo ilifanya dhidi ya Muembe Makumbi City.
Yanga imeonyesha kutokuwa na mzaha kwa kuendelea kutumia kikosi chake bora licha ya ratiba ngumu, ikiwa pia inajiandaa na mchezo mkubwa wa ligi dhidi ya Simba Mei 3.
Kwa upande wa Azam, timu hiyo imeonyesha nia ya kweli ya kulichukua kombe hili baada ya kuwapumzisha baadhi ya mastaa wake muhimu katika mechi iliyopita.
Wachezaji kama Feisal Salum ‘Fei Toto’, Idd Seleman ‘Nado’, kipa Aishi Manula pamoja na mabeki Lusajo Mwaikenda na Fuentes Mendoza wanatarajiwa kurejea kikosini leo.
Washambuliaji Prince Dube na Jean Ngita ndio vinara wa mabao kwenye mashindano haya, kila mmoja akiwa na mabao mawili.
Vita nyingine itakuwa eneo la kiungo ambapo endapo Fei Toto atakuwa uwanjani anayeongoza kwa asisti kule ligi kuu akiwa nazo saba, basi kuna uwezekano watakumbushia tena mbio zao za kutengeneza asisti kati yake na Allan Okello wa Yanga ambaye kwenye mashindano haya tayari anayo moja. Kwenye ligi anazo sita, moja nyuma ya Fei Toto.
Kwa Yanga, Duke Abuya, Mudathir Yahya, Mohamed Damaro na Maxi Nzengeli wanatarajiwa kuongoza eneo la kati.
Azam chini ya Ibenge, tunaweza kuona sapraizi huenda atampa nafasi Adolf Mtasingwa ambaye sasa yupo fiti baada ya kupona majeraha na tayari amecheza dhidi ya KVZ, pia mkata umeme mwingine, Sadio Kanoute yupo tayari kwa mapambano.
Kwa ubora wa majina haya, eneo la kiungo linaonekana kuwa uwanja wa mapambano makali kati ya wakabaji na watengenezaji wa mashambulizi, hali itakayoweza kuamua matokeo ya mechi.
WASIKIE WENYEWE
Kocha wa Azam, Florent Ibenge alisema:
“Kesho (leo) ni mchezo mkubwa kila mmoja anajua kwa sasa kwenye ligi yetu kule Yanga ndio timu bora kwa takwimu, sisi Azam tunafahamu tunakwenda kukutana na timu ngumu yenye hadhi hiyo kwenye mchezo wa nusu fainali,” amesemaIbenge.
“Sisi (Azam) tunapenda kucheza mechi ngumu kama hizi, nawapongeza sana wachezaji wangu kwa kujituma na kufikia hatua hii, tumejiandaa kucheza kama ambavyo tumekuwa tukicheza, tutawapa nafasi wachezaji ambao tunaamini wataweza kutupa matokeo mazuri, najivunia wachezaji wangu haijalishi ni vijana au wale wakongwe.”
Kocha wa Yanga, Pedro Goncalves alisema:
“Kesho (leo) ni nusu fainali tutakutana na Azam FC, moja ya timu bora zinazowania mataji hapa Tanzania, ni timu yenye nguvu, iliyofanya uwekezaji mkubwa, wanaohtaji mashindano kama haya kuthibitisha ubora wao, yenye wachezaji wazuri na kocha mwenye wasifu mkubwa kwenye soka la Afrika,” amesemaGoncalves.
“Tunatarajia mchezo mgumu, tunatakiwa kuwa tayari kukabiliana nao, tunapita kwenye ratiba ngumu ya mashindano, sasa tuna mchezo wa nusu fainali na baada ya hapo tukishinda tutakwenda kwenye fainali tukimaliza mashindano haya tutakuwa na mchezo mgumu wa ligi dhidi ya Simba, lakini ni motisha kwetu kucheza dhidi ya wapinzani wetu wakubwa, tukiwa na akili ya kushinda hizo mechi.”
