KOCHA Mkuu wa Azam FC, Florent Ibenge, amesema kikosi chake kinafahamu vizuri ubora wa Simba, huku akisisitiza kuwa mchezo wao wa leo utakuwa na hadhi ya kimataifa kutokana na uzoefu wa timu zote mbili kwenye michuano ya Afrika.
Azam FC itakuwa mwenyeji wa pambano hilo dhidi ya Simba, litakalopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam, ambapo mashabiki wanatarajia kushuhudia ushindani mkali.
Ibenge ameeleza kuwa Simba si timu ndogo, na ndio maana wanauchukulia mchezo huo kwa uzito mkubwa, akiuona kama mechi yenye ladha ya kimataifa kutokana na historia ya hivi karibuni ya timu hizo katika mashindano ya Afrika.
Amefafanua kuwa Simba ilishiriki hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, wakati Azam FC nayo ilifika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika, jambo linaloonyesha ubora wa pande zote mbili.
“Hautakuwa mchezo rahisi hata kidogo. Tunautambua ubora na ukubwa wa Simba, lakini sisi pia tupo tayari kupambana. Hii ni mechi yenye hadhi ya Afrika,” amesema Ibenge.
