Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini Misri (EFA) limewasimamisha kazi kwa muda usiojulikana mwamuzi na wasaidizi wake waliohusika katika mchezo wa daraja la pili kati ya Tanta na Telecom Egypt, kufuatia kitendo cha ajabu cha kutumia simu ya mkononi kama “VAR ya mchongo”. Katika hali iliyozua mshangao, mwamuzi huyo alionekana akitumia simu ya mmoja wa watu waliokuwa karibu na uwanja kupitia upya picha za video za tukio la penalti iliyokuwa na utata. Baada ya kujiridhisha kupitia kioo cha simu hiyo, mwamuzi huyo aliamua kufuta maamuzi ya awali ya penalti, jambo ambalo ni kinyume kabisa na taratibu za mpira wa miguu duniani.
Tukio hilo limetajwa kama moja ya matukio ya ajabu zaidi kuwahi kushuhudiwa katika soka la Afrika, likizua mjadala mzito kuhusu matumizi ya teknolojia uwanjani. Shirikisho la Misri tayari limeanzisha uchunguzi wa kina kubaini simu hiyo ilikuwa ya nani na jinsi ilivyofika mikononi mwa mwamuzi katikati ya mchezo. Wakati wachambuzi wa soka wakicheka na kusema “soka la Afrika halichoshi”, mamlaka za soka nchini Misri zimechukua hatua hiyo ya dharura kulinda hadhi ya mchezo huo, huku zikisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia lazima yafuate kanuni rasmi za FIFA na CAF.
