Afisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe, amewatoa hofu mashabiki wa klabu hiyo kufuatia kupoteza fainali ya Muungano Cup 2026 dhidi ya Simba SC. Kamwe amewasisitiza mashabiki kutokata tamaa, akieleza kuwa mchezo huo haupaswi kupewa uzito mkubwa kwani ulikuwa na sura ya kirafiki, na badala yake nguvu zote zielekezwe kwenye mashindano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kupitia ujumbe wake, Kamwe amewataka wachezaji na mashabiki kuinua vichwa juu licha ya matokeo hayo, akiamini kuwa timu bado ina kikosi imara chenye uwezo wa kukabiliana na presha na kurejea kwenye ubora wake.
Amesema kuwa ni kawaida kwa timu kukutana na changamoto kama uchovu, hasira na huzuni, lakini hali hizo ndizo zinazojenga timu imara zaidi. Ameongeza kuwa ni muhimu sasa kurejea mazoezini, kufanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza, na kuendelea kupambana ili kutetea ubingwa wa ligi.
Kamwe pia amesisitiza kuwa ana imani kubwa na wachezaji wa Yanga, akieleza kuwa wana uwezo wa kushinda changamoto hiyo na kuendelea kufanya vizuri katika michezo ijayo.
Amehitimisha kwa kuwataka mashabiki kuendelea kuwaunga mkono wachezaji na kubaki na kauli mbiu yao ya “Daima Mbele, Nyuma Mwiko.”
